Monday, August 23, 2010

Kumbe walilipwa kuhudhuria mkutano wa CCM Dar!






Wananchi wengi katika umati mkubwa wa watu waliohudhuria mkutano wa uzinduzi wa kampeni za CCM kule Jangwani siku ya Jumamosi iliyopita walifika hapo baada ya kuliupwa kufanya hivyo.



Baadhi ya watu niliozungumza nao wanaotoka sehemu za Mbagala Rangi Tatu na Mbande wanasema mabasi ya daladala yalikodishwa na CCM kusomba watu kuwaleta jijini kuhudhuria mkutano na waliokubali kupanda walilipwa Sh 5,000 kwamba hizo fedha ni za usumbufu na nauli yao ya kurudi baada ya mkutano.



Kila moja ya mabasi haya yaliyokodishwa yalikuwa yanalipwa mapato yao ya siku mbili.





WanaJF, hizi habari ni za uhakika nilizopata kutoka kwa watu watatu waliopanda mabasi hayo na kulipwa kutoka sehemu hizo mbili nilizotaja. Wanasema tangu asubuhi majira ya saa 3 mabasi yalifika maeneo hayo na kuegesha huku viongozi na makada wa CCM wakihamasisha watu kuingia. Sh 5,000 ni nyingi sana katika sehemu hizo.



Hali hii bila shaka ilijitokeza katika sehemu nyingi tu pembezoni mwa Jiji siku hiyo – watu kulipwa na kutafutiwa usafiri ili wahudhurie mkutano.



Mapesa yaliyotumika ni mengi kwa tafsiri yoyote ile, na bila shaka ni kati ya zile Sh Bilioni 50 ambazo CCM imetenga kwa ajili ya kampeni mwaka huu.



Tatizo langu hapa si uhalali au la kwa CCM kulipa watu kuhudhuria mkutano wao wa kampeni, ingawa pengine ni suala linaloweza kutazamwa kama ni njia mojawapo ya kuwahonga wapiga kura.



Tatizo langu hasa ni ile dhana inayojengwa kwamba CCM bado ina wafuasi wengi, dhana ambayo siyo kweli kwani iwapo wananchi wangeachwa kufika hiari yao, mkutano ule ungehudhuriwa labda na nusu tu ya watu waliojitokeza.



Wanachofanya CCM ni kujenga muonekano wa ufuasi mkubwa katika mikutano yao kwa nguvu fedha walizonazo – na siyo kwa hiari ya wananchi wenyewe bila kushawishia kwa njia ya pesa.

No comments:

Post a Comment