Friday, August 20, 2010

Rais Kikwete na Wafanyakazi


Madai ya wafanyakazi kutaka nyongeza ya mshahara yalianza muda mrefu, kiwango hicho ambazo Rais Kikwete amekitaja leo kwa dhihaka kilianza kuzungumziwa toka mwaka 2007; ni hatua gani serikali yake ilichukua toka wakati huo mpaka wakati huu?

Hotuba ya Rais imenifanya nikumbuke makala hii ambayo niliindika mwaka 2007: http://www.chadema.or.tz/makala/makala.php?id=51



Katika makala hiyo nilinukuu kipande cha hotuba ya Nyerere ambacho ni muhimu nikakirejea hivi sasa katika muktadha wa Hotuba ya Kikwete.

Mwalimu Nyerere yeye alikabiliana moja kwa moja na wahuhusika na kuwaeleza: “Mna haki mnapozungumzia mishahara…..mishahara yetu ipo juu sana. Mnataka niipunguze? (makofi)…..mnataka nianzie na mshahara wangu? Ndio, naanza kuukata wa kwangu (vilio vya ‘hapana’). Nitapunguuza hii mishahara katika nchi hii. Wangu naukata kwa asilimia ishirini kuanzia sasa…..hii mishahara hii. Hii mishahara ndio inajenga huu mtazamo kwa wasomi, wote kabisa. Mimi na wewe. Tuko katika tabaka la wanyonyaji. Niko katika tabaka lenu. Ambapo nafikiri paundi mia tatu na themanini kwa mwaka (kiwango cha chini cha mshahara uliokuwa ukilipwa katika Jeshi la Kujenga Taifa) ni kambi ya gereza, ni kufanyishwa kazi kwa shuruti. Tuko katika tabaka la juu la wanyonyaji. Je hiki ndicho ambacho taifa letu kilipigania? Je hiki ndicho tulichokihangaikia? Ili tuendeleze tabaka la juu la wanyonyaji?....mko sawa, mishahara ipo juu sana. Kila mtu katika nchi hii anahitaji paundi ya ziada. Kila mtu isipokuwa mkulima masikini. Anawezaje kutaka? Haijui lugha…je ni nchi ya namna gani tunajenga?” (tafsiri yangu toka nukuu ya hotuba ya kingereza ya Hayati Baba wa Taifa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere aliitoa papo kwa papo akizungumza na wanafunzi wa Chuo cha Dar es Salaam baada ya maandamano ya wanafunzi Oktoba mwaka 1966)

Nyerere wakati huo alikwenda kuihutubia hadhira muafaka kwa suala alilolizungumzia, lakini kwa Kikwete yeye alikwenda kuwahutubia wazee na kuhusu ‘wafanyakazi’; je, alikuwa anapeleka mashtaka au alikuwa anatafuta kupigiwa makofi na hadhira isiyohusika ama ni ishara ya hofu ya kuogopa kukabiliana na wafanyakazi ana kwa ana?

Kuhusu Hotuba la Rais kusema kwamba mgomo ni batili anapewa taarifa nusu nusu au anapotoshwa ama ameamua kuupotosha umma. Ni vizuri serikali ikarejea na kukumbuka kuwa kusudio la mgomo lilitolewa siku nyingi nyuma kama sheria inavyohitaji; na wafanyakazi walieleza wazi kwamba walirejea kwenye majadiliano kwa maombi ya umma huku kusudio lao likiwepo pale pale. Hivyo, ni muhimu serikali ikaepusha mgomo kwa kushughulikia madai ya msingi ya wafanyakazi ambayo ni nyongeza ya mshahara hususani kima cha chini, punguzo la makato ya kodi na uboreshaji wa pensheni wakati wa kustaafu. Nilisoma tangazo la baraza husika ambalo limeshapwa na serikali katika magazeti mbalimbali hivi karibuni lilieleza bayana kwamba katika suala la kiwango cha kima cha chini 'wamekubaliana kutokukubaliana'; hivyo nimeshangazwa na kauli ya Rais Kikwete ya kwamba majadiliano yalifikia makubaliano kuhusu kiwango.



Tafsiri ya matukio haya ni ama kuna ufa mkali ndani ya serikali ama serikali imekerwa na kutoalikwa Mei Mosi huku ikijaribu kutumia kila mbinu kuficha aibu ya mgomo wa wafanyakazi wakati nchi ikiwa mwenyeji wa World Economic Forum-Africa(mbinu waliyoitumia kupanda miti mikubwa ya haraka haraka along Sam Nujoma Road).



Lakini naamini Rais anatambua kwamba watu wachache wanaweza kudanganywa kwa muda mchache, lakini sio watu watu wakati wote. Jaribio la hotuba ya Rais kuwatweza viongozi wafanyakazi linaweza likaishia kuwakweza zaidi, jaribio la kuwachangonanisha wafanyakazi kuwa wanataka mishahara mikubwa wakati serikali inahitaji fedha za kutoa huduma kwa jamii ili wananchi wawajie juu wafanyakazi kuwa wanajipendelea nalo limeelekea kushindwa. Jaribu la kuwachonganisha wafanyakazi kwa wafanyakazi, wafanyabiashara kwa wafanyakazi( kwa kutumia mifano ya mwenye baa na mifano ya house girl) nalo limeelekea kupuuzwa. Taasisi ya Urais sio idara ya propaganda za kutumia kejeli ama uchonganishi; Rais alipaswa kujenga hoja, kutoa matumaini na kutoa uongozi mbadala.



Hasira alizozionyesha kwa TUCTA ndio amekuwa amezionyesha kwa kiwango hicho hicho kwa mafisadi, na nguvu hizo hizo za kuzima hoja angekuwa amezitumia kwenye kutoa uongozi bora na kusimamia vizuri rasilimali za taifa mapato ya serikali yangewezesha kuwa na nyongeza ya mishahara kwa wafanyakazi na ukuaji wa uchumi ungewezesha hata kukuka kwa kipato katika sekta binafsi huku mfumuko wa bei ungedhibitiwa kwa kiwango cha kuridhisha. Wakati wafanyakazi wanaendelea kutozwa kodi kubwa(dai ambalo Rais hakulizungumzia), ni serikali yake hii ambayo iko mstari wa mbele kutoa katika mazingira ya utata misamaha mikubwa ya kodi.



Kama divide and rule hii ikiindelea kwa kiwango cha wafanyakazi kushindwa kushikamana, bado kila mmoja anayo fursa ya kugoma kumpa kura (kwanza ameshatangaza mwenyewe kuwa kura hazitaki). Upo msemo kwamba madaraka hulevya, na madaraka zaidi hulevya zaidi; unapokuwa na taifa lenye hodhi (monopoly) ya chama kimoja katika vyombo vya maamuzi; si ajabu kupata kauli za namna hii. Hii ndio athari ya kura zilizoitwa za mafiga matatu; lakini ipo fursa bado ya kubadili mfumo wa utawala ili tuwe na uwajibikaji wa kutosha si kwenye sererikali tu, hata kwenye taasisi zingine ikiwemo vyama vya wafanyakazi vyenyewe.



Kwa walio nje ya ajira zenye malipo duni suala hili wanaweza wakaona haliwahusu, lakini ukweli ni kuwa kuna uhusiano mkubwa katika ya ubovu wa huduma tunazozipata kwenye sekta mbalimbali na hali duni katika sekta hizo; hili ni bomu la wakati. Wafanyakazi wa Tanzania wamekuwa wawafanyi migomo rasmi kama nchi nyingine duniani, lakini aina ya mgomo unaoendelea chini kwa chini nchini ni mbaya zaidi kwa mustakabali wa nchi yetu. Tanzania kuna mgomo wa kutokuwajibika, katika hususani katika utumishi wa umma; wapo wanaokwenda kazini mwaka mzima lakini wanafanya kazi masaa machache au siku chache; muda mwingine kwenye warsha/semina kufidia kipato duni wanachopata ama muda mwingi zaidi kwenye shughuli zao binafsi. Mfano; walimu wenye wanaofundisha masomo ya ziada (tuition) ama kufanya biashara za visheti kwa wanafunzi shuleni; ama daktari anayetumia muda mwingi zaidi kwenye shughuli binafsi kuliko ndani ya hospitali ya umma, sasa 'consultancy' ndani ya serikali kwa serikali ndio zimekuwa utamaduni wa kawaida.



Rais atangaze mshahara wake hadharani na atueleze baraza lake la mawaziri limeshughulikiaje madai makuu matatu ya wafanyakazi toka aingine madarakani mwaka 2005 badala ya kukimbilia kuwapa jina baya viongozi wa wafanyakazi kuwa 'wanatumiwa'. Kama kweli wanatumiwa atueleze wanatumiwa na nani kwa kwanini? Na yeye na serikali yake waulizwe 'wanatumiwa na nani' au wanamtumikia nani?

Posted by John Mnyika at 5:43 AM 0 comments Links to this post

Thursday, April 15, 2010

Mnyika: Uhamisho wa watumishi Mwananyamala ni wa kisiasa

Mnyika: Uhamisho wa watumishi Mwananyamala ni wa kisiasa



na Lucy Ngowi



MWENYEKITI wa Mkoa wa Kinondoni, Kanda Maalumu ya Dar es Salaam kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), John Mnyika, amesema suala la kuwahamisha watumishi 96 katika Hospitali ya Mwananyamala limefanywa kisiasa zaidi katika kipindi hiki kinachoelekea Uchaguzi Mkuu.



Mnyika alisema hayo katika taarifa yake kwa vyombo vya habari na kuongeza kuwa analiona suala hilo lipo kisiasa zaidi kwa kuwa hatua hiyo iliyochukuliwa imechelewa, kwani wananchi na vyama vya siasa wamekuwa wakililalamikia tangu mwaka 2005.



Mnyika ambaye ni Mkurugenzi wa Vijana wa CHADEMA, alisema upunguzaji huo si suluhisho la kudumu, ila kiutawala ni hatua inayopunguza tatizo kwa muda mfupi.

Kwa mujibu wa Mnyika, hatua ambazo zilipaswa kuchukuliwa ni pamoja na kubadili mfumo mzima wa utoaji huduma katika hospitali za umma kwa kubadili uongozi na kuongeza masilahi ya watumishi wa sekta hiyo.



Mkurugenzi huyo wa vijana alisema kuwa hatua nyingine ni pamoja na kuboresha huduma kwa wananchi, hususan upatikanaji wa dawa.



“Kuhamisha bila kushughulikia kero za msingi ni sawa na kiini macho. Serikali iweke wazi ripoti za tume na kamati zote zilizoundwa kuchunguza matukio yaliyokuwa yanajitokeza toka wakati huo, pamoja na kueleza gharama zilizotumiwa na tume ama kamati hizo bila mapendekezo kutekelezwa kwa ukamilifu,” alisema.



Mwanzoni mwa wiki hii, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, William Lukuvi, alisema kuwa, serikali imewahamisha watumishi 96 katika Hospitali ya Mwananyamala ambayo kwa muda mrefu imekuwa ikilalamikiwa kwa uzembe.



Chanzo: http://www.freemedia.co.tz/daima/habari.php?id=14932

Posted by John Mnyika at 11:51 AM 0 comments Links to this post

Thursday, March 25, 2010

Tamko letu kuhusu ajali ya leo Kata ya Kibamba Wilaya ya Kinondoni

Taarifa kwa Umma: Kwa niaba ya Uongozi wa CHADEMA Mkoa wa Kinondoni Kanda Maalum ya Dar es salaam; natuma salamu za rambi rambi kwa ndugu, jamaa na marafiki wa wafiwa wote kufuatia ajali mbaya iliyotokea leo asubuhi Kibamba jijini Dar es salaam ikihusisha Lori la Mafuta na Hiece iliyokuwa na abiria.



Aidha tunatoa mwito kwa serikali na vyombo vya dola kufanya uchunguzi wa kina kuhusu vyanzo vya ajali za mara kwa mara katika eneo la Kibamba ambazo zimekuwa zikisababisha vifo, majeruhi na uharibifu wa mali.



Ikumbukwe kuwa mwezi Disemba mwaka 2007 ajali nyingine ilitokea eneo la Kibamba Hospital ikihusisha malori na kusababisha vifo vya watu saba akiwemo mjamzito na wengine 11 kujeruhiwa.



Aidha mwezi Aprili 2008 Bunge jumla ya watu 181 wamepoteza maisha kwa kugongwa na magari kati ya mwaka 2005 hadi mwaka 2007 katika eneo la kuanzia Kibamba mpaka Ubungo kwenye mataa.



Ikumbukwe kuwa Mei 2009 madereva wawili walikufa baada ya magari yao kugongana uso kwa uso huko maeneo hayo hayo ya Kibamba.

Itakumbukwa pia kwamba mwezi Januari 2010 watu 18 walijeruhiwa vibaya katika ajali ya gari iliyotokea katika barabara ya Morogoro eneo la Kibamba Darajani (barabara ina mteremko kuelekea darajani) ambapo magari matano yaligongana kwa pamoja.



Imetolewa tarehe 25 Machi 2010:











John Mnyika-0754694553; mnyika@chadema.or.tz

Mwenyekiti wa Mkoa wa Kinondoni Kanda Maalum (CHADEMA)













Posted by John Mnyika at 3:31 AM 0 comments Links to this post

Saturday, March 20, 2010

Natangaza rasmi dhamira ya kugombea ubunge 2010

Ni wakati wa mabadiliko ya kweli; tuwajibike



Utangulizi



Wapendwa wananchi wezangu na marafiki zangu ndani na nje ya jimbo la Ubungo. Ninayofuraha kuwatangazia rasmi dhamira yangu ya kugombea ubunge katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu. Nimefikia uamuzi huu baada ya kusikia maoni ya wengi wenu na kuisikiliza pia nafsi yangu katika kipindi cha kuanzia mwishoni mwa mwaka 2009 mpaka mwanzoni mwa mwaka 2010. Wakati wa kampeni bado, hivyo sitazungumzia kwa sasa ahadi zangu kwenu wala ilani ya chama; lakini inatosha kuwaambia tu kwamba: ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike. Naamini katika kuwa na uongozi bora wenye dira na uadilifu wa kuwezesha uwajibikaji katika kusimamia rasilimali za umma ikiwemo kodi zetu na mali asili za nchi yetu kwa ajili ya kujenga taifa lenye kutoa fursa kwa wote.





Nautambua wajibu; tushirikiane



Naamini kwamba mbunge (ambaye pia kwa nafasi yake ni diwani katika halmashauri) ana wajibu katika maeneo makuu manne (kwa kadiri ya umuhimu).



Mosi; kusikiliza na kuwakilisha wananchi, Pili; kuisimamia na kuiwajibisha serikali na viongozi wake, Tatu; kushiriki katika kutunga sheria, Nne; kuhamasisha upatikanaji wa huduma.



Hata hivyo, sehemu kubwa ya wabunge wetu hawaweki kipaumbele katika majukumu ya kwanza matatu ambayo ndio msingi wa ubunge wenyewe. Matokeo yake ni matakwa ya wananchi kutokuwakilishwa kikamilifu, ufisadi, rushwa, matumizi mabaya ya madaraka na mikataba mibovu; uwepo wa sheria dhaifu na kutetereka kwa utawala wa sheria na mifumo ya haki masuala ambayo yanakwaza jitihada za maendeleo za wananchi binafsi za taifa kwa ujumla.



Wabunge wengi wanawaza kwamba jukumu kubwa la mbunge ni kutoa bidhaa na huduma kwa wananchi; wakiacha taifa katika lindi la umasikini na kufanya sehemu ya wananchi kujenga mazoea ya kutegemea hisani toka kwa viongozi wa umma na wafadhili wao.



Mwaka 2005 pamoja na majukumu hayo makuu matatu, nilizungumzia suala la mfuko wa maendeleo ya jimbo. Lakini si katika mwelekeo wa mfuko wa sasa uliopitishwa kuwa sheria unaosubiriwa kutungiwa kanuni. Kwa hiyo, wakati nikiunga mkono jukumu la mbunge kuhamasisha maendeleo na kushiriki kwenye shughuli za kijamii, siamini katika mazoea na mfumo wowote unaomfanya mbunge kuwa “mtoa bidhaa na huduma” (mithili ya ATM) kwani unarutubisha ufisadi wa kisiasa na kuhatarisha mwelekeo mzima wa utawala bora. Kama ambavyo siamini pia katika siasa chafu za rushwa, uongo na aina nyingine ya upofu wa kimaadili katika kampeni na uongozi kwa ujumla.



Haiwezekani wakati ambapo makisio yanaonyesha kwamba zaidi ya trilioni mbili (sawa na milioni milioni mbili) zinapotea kila mwaka kupitia misamaha ya kodi, upangaji bei hovyo kwa bidhaa za Tanzania, biashara haramu kati ya Tanzania na nchi za nje au makampuni ya kimataifa halafu wananchi wakubali kupumbazwa na bidhaa za milioni chache zinatolewa na viongozi wa umma walioshindwa kurekebisha hali hii.



Nilisema wakati wa uchaguzi wa mwaka 2005, na narudia leo. Kipaumbele cha wananchi wa Jimbo la Ubungo ni kupata mbunge mkweli, mwadilifu, mwajibikaji, mwenye dira, atayewasilikiliza na kuwawakilisha ipasavyo. Iwe ni wananchi wa Kwembe, Mloganzila na maeneo mengine yenye migogoro ya ardhi. Ama wale wa Saranga, Baruti na kwingineko kwenye matatizo ya maji huku mabomba makubwa ya maji yakipita jimboni na uwepo wa Chuo cha Maji, na Wizara ya Maji ndani ya jimbo letu. Iwe ni wale Bonyokwa, Mpiji Magoe na kote kwenye udhaifu wa mipango miji na matatizo ya usafiri huku Chuo cha Usafishaji cha Taifa kikiwa ndani ya jimbo hili hili.



Iwe ni wafanyakazi wa Kiwanda cha Urafiki hapa Ubungo ama wa sekta umma na wa binafsi waoishi ndani ya jimbo hili wenye kubebeshwa mzigo mkubwa wa kodi na kuzongwa na maslahi duni. Iwe ni wafanyabiashara ndogo ndogo wanawake kwa vijana pale Manzese, Makurumla na kwingineko; iwe ni wanafunzi wa sekondari na vyuo Mbezi na Ubungo ambao kwa ujumla wake wanaishi katika mazingira yenye mifumo dhaifu yenye kudorora kwa ubora na upatikanaji nafuu wa huduma za kijamii.



Iwe ni mwananchi wa Jimbo la Ubungo anayeathirika kwa bei na mgawo wa umeme huku akipita na kuona mitambo ya kampuni feki ya Dowans inayotakiwa kurejesha mabilioni iliyolipwa mara mbili (double payment) na serikali; mitambo ambayo imeendelea kukaa pembeni na makao makuu ya TANESCO yaliyopo jimbo la Ubungo bila kutaifishwa. Iwe ni mtanzania wa kawaida anayeelemewa na mzigo wa kodi na kupanda kwa gharama za maisha. Wote wanahitaji mbunge wa kuwasikiliza, kuwawakilisha, kushiriki kutunga sheria bora na kuziwajibisha mamlaka zinazohusika. Tanzania bila mafisadi inawezekana. Huu si wakati wa kuahidi nitafanya nini kwa kuwa si kipindi cha kampeni. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.





Tunahitaji mabadiliko ya kweli kuliko ahadi kedekede utekelezaji legelege



Natambua kwamba Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977 (pamoja na ubovu wake) imetaja katika ibara ya 9 Mamlaka ya Nchi na vyombo vyake vyote vinawajibika kuelekeza sera na shughuli zake zote katika lengo la kuhakikisha: kwamba utu na haki nyinginezo zote za binadamu zinaheshimiwa na kuthaminiwa; kwamba sheria za nchi zinalindwa na kutekelezwa; kwamba shughuli za Serikali zinatekelezwa kwa njia ambazo zitahakikisha kwamba utajiri wa Taifa unaendelezwa, unahifadhiwa na unatumiwa kwa manufaa ya wananchi wote kwa jumla na pia kuzuia mtu kumyonya mtu mwingine; kwamba maendeleo ya uchumi wa Taifa yanakuzwa na kupangwa kwa ulinganifu na kwa pamoja; kwamba aina zote za dhuluma, vitisho, ubaguzi, rushwa, uonevu au upendeleo zinaondolewa nchini; kwamba matumizi ya utajiri wa Taifa yanatilia mkazo maendeleo ya wananchi na hasa zaidi yanaelekezwa kwenye jitihada ya kuondosha umaskini, ujinga na maradhi. Misingi hii na mingine, haitekelezwi wala kuzingatiwa kikamilifu kutokana na ombwe la uongozi, udhaifu wa kitaasisi na upungufu wa uwajibikaji. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.



Aidha naelewa kuwa katiba hiyo hiyo (pamoja na mapungufu yake) inatamka katika Ibara ya 63 kifungu cha pili na cha tatu kuwa Bunge ndicho chombo kikuu cha Jamhuri ya Muungano ambacho kitakuwa na madaraka, kwa niaba ya wananchi, kuisimamia na kuishauri Serikali ya Jamhuri ya Muungano na vyombo vyake vyote katika utekelezaji wa majukumu yake kupitia maswali, mijadala, kuidhinisha mipango (zikiwemo bajeti), kutunga sheria na kuridhia mikataba.



Madaraka hayo ya bunge na majukumu ya wabunge hata baada ya uongozi wa awamu ya nne kuahidi kuyatekeleza kwa ari, nguvu na kasi mpya na Spika wa Bunge kuahidi kuyasimamia kwa kasi na viwango; hali kwa sehemu kubwa iko vile vile; ahadi kedekede, utekelezaji lege lege.



Hasara kwa taifa iliyotajwa kwenye orodha ya mafisadi (list of shame) na ile inayotokana na ufisadi kwenye serikali za mitaa pekee kwa ujumla wake inafikia takribani trilioni mbili. Hivyo Tanzania ni nchi tajiri wa rasilimali huku wananchi walio wengi wakiishi katika lindi la umasikini na ugumu wa maisha.



Naamini hali hii inachangiwa na kufilisika kiitikadi na kidira kwa chama tawala, hodhi (monopoly) ya chama kimoja bungeni, bunge kukosa uhuru wa kikatiba na udhaifu wa taasisi za kusimamia uwajibikaji. Hali hii inachochewa pia na udhaifu wa kiuongozi ikiwemo uzembe wa sehemu kubwa ya wabunge wengi wao wakiwa wameingia kwa nguvu ya ufisadi katika uchaguzi wa mwaka 2005 na hivyo kukosa nguvu ya kimaadili na dhamira ya kuleta mabadiliko ya kweli. Hata wale wachache wenye dhamira ya kufanya mabadiliko wanadhibitiwa na kamati za chama chao (party caucus) chenye mmomonyoko wa kimaadili. Hivyo, harakati za ukombozi zinapaswa kuungwa mkono na watanzania wote wakiwemo wanachama wa chama hicho wanaokerwa na hali ya mambo. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.





Tuchukue hatua; kwa pamoja tunaweza



Jukumu lililo mbele yetu la kuwezesha mabadiliko ya kweli ni kubwa linalohitaji hatua za haraka kujitoa sadaka na kutumia talanta kuanzia sasa mpaka wakati wa uchaguzi Oktoba 2010; kabla ya majukumu makubwa zaidi kuanzia wakati huo na kuendelea. Kwa pamoja tunaweza, pamoja tutashinda.



Hatua ya kwanza ni kuhakikisha kila mmoja mwenye umri wa miaka 18 na kuendelea ama atayefikisha umri huo wakati wa uchaguzi kama bado hajajiandikisha anajitokeza kujiandikisha katika uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura unaonza katika Mkoa wa Dar es salaam kuanzia kesho tarehe 22 mpaka 27 Machi, 2010 ikiwa ni awamu ya mwisho kabla ya uchaguzi mkuu. Aidha kwa waliohama makazi, huu ndio wasaa mwafaka pia wa kwenda kubadilisha taarifa zenu ili muweze kupiga kura katika maeneo mliyopo.



Hatua ya pili ni kushiriki kwa hali na mali katika kujenga oganizesheni ya chama mbadala. Kuhamasisha wagombea mbadala kujitokeza kugombea katika nafasi mbalimbali, kuwaunga mkono na kueneza ujumbe wa matumaini wa mabadiliko kwa watanzania wengine katika maeneo yenu. Izingatiwe kuwa kipindi cha kuanzia mwezi Aprili mpaka Julai ni cha wagombea kuonyesha nia, kuchukua fomu ndani ya vyama, kampeni za ndani ya vyama, kuingia katika kura za maoni na uteuzi kufanywa na vyama vyao kwa kuwa serikali mpaka hivi sasa imekataa matakwa ya umma ya kutaka wagombea binafsi waruhusiwe.



Kampeni kwa umma zinatarajiwa kuanza baada ya wagombea kuteuliwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi mwezi Agosti na zinatarajiwa kukamilika mwezi Oktoba mwaka 2010. Hatua muhimu wakati huo ni pamoja na kushiriki katika kampeni kwa hali na mali, kupiga kura na kuunganisha nguvu ya umma katika kulinda kura. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.



Haturudi nyuma kamwe; matumaini yapo mbele



Mwaka 2005 Mwezi Machi kama huu nilipochukua fomu kwa mara ya kwanza kugombea ubunge, CHADEMA haikuwa na mtandao imara katika jimbo la Ubungo tofauti na sasa ambapo ina mtandao madhubuti na ipo fursa bado ya kuufanya kuwa mzuri zaidi. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.



Hivyo Disemba 2005 (pamoja na kukubalika kwa wananchi) baada ya mvutano wa siku kadhaa matokeo ya uchaguzi yalitangazwa kwa shuruti bila kupitia utaratibu wa kupitia na kujumlisha kituo hadi kituo na kufanya jumla ya wapiga kura waliotangazwa kupiga kura katika ubunge kuzidi wale waliopiga kura za urais kwa zaidi ya kura elfu thelathini (30,000) katika uchaguzi uliofanyika katika siku moja.



Kutokana na hujuma hizo na nyinginezo zilizohusisha pia ufisadi katika uchaguzi niliamua kufungua kesi namba moja ya mwaka 2006 katika Mahakama Kuu kupinga matokeo hayo. Kesi ambayo kwa miaka mingi imekuwa ikipigwa danadana za kiufundi bila kuingia katika kusikiliza msingi wenyewe wa kesi.



Wakati najiandaa kutangaza rasmi dhamira ya kugombea nikitazama mbele kwa matumaini, nimepokea simu toka kwa Wakili wangu katika kesi hiyo Ndugu Tundu Lissu akinieleza kwamba hatimaye Mahakama Kuu imepanga kuwa kesho tarehe 22 Machi 2010 ndio siku ambayo mahakama itatoa hukumu juu ya kesi hiyo.



Bila kuingilia uhuru wa mahakama, nieleze wazi tu kwamba kwa mtiririko wa mambo mpaka sasa hukumu hiyo itahusu zaidi ombi langu la kuondolewa kuweka dhamana ya milioni tano kama sharti la kufungua kesi na kupita kwa muda toka kesi ifunguliwe badala ya utata wa matokeo na kasoro za uchaguzi husika.



Hata hivyo kwa miaka takribani mitano ambayo nimekuwepo katika siasa na kushiriki katika chaguzi mbalimbali za kiserikali, mmoja nikiwa kama mgombea na zingine nikiwa kwenye timu za kampeni nimejifunza kuwa pamoja na uwepo wa katiba na sheria mbovu zenye kusababisha tume ya uchaguzi kutokuwa huru na kukosekana kwa uwanja sawa wa kisiasa kwa ujumla; bado vyama mbadala vinaweza kuunganisha nguvu ya umma kupata kura nyingi na kushinikiza mshindi kutangazwa pale ambapo kunakuwa na mikakati thabiti, oganizesheni makini na uongozi mahiri. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.



Naweza nikalazimika kutangaza upande wa kugombea



Tunahitaji mabadiliko ya uongozi na mfumo wa utawala ili kutumia vizuri kodi za wananchi na rasilimali za taifa kuwa na miundo mbinu ya kisiasa, kiuchumi na kijamii kuwezesha ustawi wa wananchi.



Badala ya kuelekeza nguvu zaidi katika azma hii, serikali ya sasa inaongeza nguvu katika matumizi ya anasa na mzigo mkubwa wa gharama za utawala na sasa inajadili kuongeza zaidi idadi ya wabunge.



Mathalani mwaka wa fedha 2009/2010 kiasi cha bajeti kilichotengwa kwa ajili ya Bunge ni shilingi bilioni 62 ambayo ni sawa na wastani wa zaidi ya milioni 190 kwa kila mbunge kwa mwaka. (Pato la mtumishi wa umma wa kima cha chini halifiki hata asilimia 1% ya fedha hizo).



Ndio maana binafsi siungi mkono ongezeko la majimbo lisiloangalia tija na ufanisi wa wabunge katika kutimiza majukumu ya msingi ya kibunge. Kwa mtizamo wangu, tunapaswa kupunguza idadi ya majimbo ya uchaguzi badala ya kuyaongeza kwa kufanya wilaya za sasa za kiutawala ndio ziwe kitovu cha mgawanyo wa majimbo.



Mathalani, wilaya ya Kinondoni badala ya kuwa na majimbo matatu ya Kawe, Kinondoni na Ubungo iwe na jimbo ni jimbo moja tu la Kinondoni. Badala yake Halmashauri ya Kinondoni bila kushirikisha vyama vya siasa ilipeleka mapendekezo kwa Baraza la Mashauriano la Mkoa (RCC) wa Dar es saaalam ambalo nalo limepeleka mapendekezo ya kugawa majimbo kadhaa ya mkoa huu likiwemo jimbo la Ubungo.



Kwa mujibu wa mapendekezo yao Kata za Kimara, Makuburi, Mbezi na Kibamba zimependekezwa kuwa kwenye jimbo la Kibamba toka Jimbo la sasa la Ubungo. Kwa msingi huo wanapendekeza sasa jimbo la Ubungo libaki na kata za Mabibo, Manzese, Makurumla, Ubungo, Sinza na Mburahati na kuongezewa pia kata ya Kigogo (ambayo kwa sasa iko ndani ya Jimbo la Kinondoni).



Kwa hiyo, pamoja na kutangaza dhamira yangu ya kugombea ubunge katika eneo ambalo ni Jimbo la Ubungo; haiwezekani kwa sasa kutangaza kwa hakika nitagombea katika jimbo gani mpaka pale Tume ya Uchaguzi itakapotangaza maamuzi yake kuhusu mgawanyo wa majimbo baada ya kupokea mapendekezo hayo toka kwa serikali. Iwapo Tume ya uchaguzi italigawa jimbo la Ubungo nitalazika kutangaza upande ambao nitagombea. Ni wakati wa mabadiliko; tuwajibike.





Hitimisho:



Maneno na matendo yangu katika harakati za umma katika kipindi cha mwaka 2000 mpaka 2005 wakati nikiwa kwenye uongozi wa kijamii katika asasi za kiraia na katika kipindi cha mwaka 2005 mpaka 2010 nikiwa kiongozi wa kisiasa yanaweza kurejewa kama msingi wa kuashiria ni watu gani nitawawakilisha na masuala gani nitayasimamia katika uongozi wa umma kabla hata sijateuliwa rasmi na kutoa hotuba katika kampeni. Naomba uwasiliane nami kwa kunitumia ujumbe kupitia johnmnyika@gmail.com au 0784222222 tuwe pamoja hatua kwa hatua katika safari ya ushindi. Ni wakati wa Mabadiliko; tuwajibike mpaka kieleweke.



Wenu katika demokrasia na maendeleo;

No comments:

Post a Comment