Kuna aina nyingi za viongozi, wapo wale ambao wao wenyewe wamejijenga (self-made) na wapo wale ambao mfumo uliopo umewajenga (epigone). JK ni matokeo ya udhaifu wa mfumo wetu wa kupata viongozi bora na wala siyo aidha jitihada zake za kufika Ikulu au ubora wa mfumo wetu wa kupata viongozi bora ndiyo umemfikisha hapo alipo. Bali JK ni mnufaikaji mahiri wa kukosekana kwa mfumo bora wa kupata viongozi bora katika uendeshaji wa Nchi hii na wala siyo vinginevyo.
Kwenye matatizo ya kimfumo ya kupata viongozi bora hili maono ya muasisi wa Taifa Baba wa taifa Mwl. Nyerere yatatuongoza hapa. Nyerere mara nyingi alikuwa akidai ili tuendele tunahitaji vitu vinne ambavyo alivibainisha ya kuwa ni watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Watu aliona ni utajiri tulionao. Ardhi hakuona ipo shida na siasa safi Nyerere aliona ni ya ujamaa na kujitegemea. (Hapa sikubaliani naye, lakini huo ni mjadala wa siku nyingine. Ni vyema mjadala huo nikauweka kiporo.) Nyerere jambo lililokuwa linamkera sana kwenye uhai wake ni kukosekana na mfumo mahiri wa kupata viongozi bora na kwa hilo yeye ni mchangiaji namba moja.
Kutokana na umangi-meza wa Nyerere, hakuwa tayari watu wenyewe maoni tofauti na yeye wakajengwa na jamii kwa minajili ya kuiendeleza bali kila alipopata nafasi aliwajenga yeye mwenyewe viongozi wabovu ambao yeye aliona kwa upeo wao mdogo angeliweza kuwatumia atakavyo bila ya bughudha yoyote ile. Hii inaelezea kwa nini Oscar Kambona alisambaratishwa baada ya kukataa siasa ya Ujamaa na kujitegemea kwa sababu haitekelezeki. Historia sasa yatufunza Kambona alikuwa sahihi na Nyerere alipotoka. Mitazamo ya Nyerere ya umangi-meza ndiyo ilizaa mfumo wa chama kimoja na kuingizwa sera za ujamaa na kujitegemea ndani ya katiba na kuwa ni za shuruti badala ya kuwa ni chaguo la wananchi. Hivi sasa, kuanzia mwaka 1992 baada ya Azimio la Zanzibar, nchi hii inakiuka katiba yake Ibara ya 9 inayotamka hadharani nchi hii ni ya kijamaa na kujitegemea wakati utandawazi na ubinafsishaji ndizo sera haramu za chama cha tawala!!!!!!!!!
Kuanzia mwaka 1992 hadi leo, CCM imekuwa ikivunja katiba kwa kubeza Ibara ya 9 inayoelekeza serikali zote za Nchi hii kujenga ujamaa na kujitegemea na wala siyo kuubeza kama inavyoendelea kwa visingizio vya utandawazi. Kanuni zipi ziwe za kuiongoza nchi zilipaswa ziamuliwe na wapiga kura kama Ibara Na. 8 ya katiba inavyotamka kuwa nchi hatima yake ipo mikononi mwa watanzania wenyewe na hivyo ni makosa kushurutisha ni mfumo upi ni sahihi kuufuata isipokuwa katika nyakati za chaguzi tu…Hili laamanisha hata Ibara za katiba zinazoruhusu mfumo wa vyama vya siasa bado una kasoro kutokana na Utangulizi (Preambles) na Ibara ya 9 kushurutisha mfumo wa ujamaa na kujitegemea kinyume na matakwa ya Ibara ya 8 ya katiba hiyohiyo!!!!!!!!!!!!!!
Umangi-meza wa Nyerere ndiyo ulisababisha vyama huru vya ushirika kufa na sasa vinaishi kwa huruma ya serikali hiyo hiyo iliyoviua!!!!!!!!!!!!
Kutokana na Nyerere kutaka kuthibiti vyombo vyote ambavyo vitatoa mtazamo mbadala wa uendeshaji matokeo yake wasomi kama JK , Lowassa. Khatibu Mohamed na wengineo wengi walipokuwa wamehitimu elimu ya Chuo kikuu hawakufikiria kwenda “uraiani” kujiendeleza kwenye elimu dunia kupitia fani zao walizozisomea la hasha bali walikimbilia kwenye chama kama njia ya mkato ya madaraka serikalini bila ya kuwa na misingi madhubuti ya taaluma zao ambazo ni muhimu katika uendeshaji wa nchi. Matokeo yake wakajikuta hawana ujuzi wowote zaidi ya kusambaza propaganda za kisiasa ambazo kiuzalishaji tija yake ni ndogo sana. Kwa vile hawakulelewa kwenye mfumo unaojali tija matokeo yake wamekuwa mstari wa mbele kutanguliza ushabiki wa kisiasa katika maamuzi ya nchi yaliyohitaji hekima za kitija zaidi. Nitafafanua zaidi hapo baadaye.
Mfumo huu wa kutanguliza ujuaji wa propoganda za chama ndio ulituletea akina Kawawa, Mwinyi, Mkapa, JK, Lowassa, Pinda na wengineo wengi ambao kigezo kikubwa cha kuyakwaa madaraka serikalini kilikuwa “huyu ni mwenzetu” na “anatosha” lakini hakuna aliyetaka wapimwe wameandaliwaje kwa kazi walizokuwa wanapigiwa debe. Mfumo huu wa kupata viongozi kutoka ndani ya chama ili wakamate dola ndiyo unaelezea kwa nini tatizo la uongozi bora alilotuachia mkoloni bado tunalo hadi kesho.
Kawawa yeye kihistoria alitoka kwenye vyama vya wafanyakazi ngazi za juu na hakuyaelewa matatizo ya wafanyakazi wa ngazi za chini matunda yake alikuwa mstari wa mbele alipokuwa sehemu ya dola katika kuminya haki za wafanyakazi hususani wa ngazi za chini. Mzee Mwinyi yeye alikuwa Mwalimu wa shule ya msingi na kupanda kwenye chati ya siasa za kitaifa kulitokana na aliyekuwa Raisi wa Zanzibar Bw. Jumbe kutofautiana na Nyerere na hivyo Nyerere kupandikiza kibaraka wake ambaye alikuwa ni Bw. Ruhksa. Mkapa alianzia vizuri kwenye tawala za mikoa na baadaye katika nyadhifa za juu kwenye vyombo vya habari za serikalini lakini kupanda vyeo vyake kulitokana na ukweli kuwa Nyerere alimfundisha na Mkapa alikuwa kijana mtiifu wa sera za Nyerere. Hakuna mahali popote pale ambapo Mkapa aliwahi kutoa changamoto ambazo zilitofautiana na Bosi wake kwa manufaa ya tija ya taifa hili. Lowassa kama alivyo JK alipohitimu elimu ya chuo kikuu alijaribu kuanzia serikalini Singida lakini baada ya muda mfupi tu changamoto alizokutana nazo zilimkimbizia chamani huko ndiko alijijengea mazingira ya kukwea vyeo AIIC, ubunge wa kuteuliwa na uwaziri na kuporomoka kwake hapa na pale zaidi kulitokana na umma kumtilia mashaka ya kuwa analamba mali za umma kwa manufaa yake binafsi. Majukumu mengi aliyobebeshwa serikalini hakuna mahali ambapo vigezo vya tija vilijidhihirisha. Mizengo Pinda ni yaleyale tu. Yeye alipomaliza chuo kikuu kituo chake cha kwanza kilikuwa ni Ikulu baada ya hapo alikwaa kazi za ukurugenzi wa Bodi ambazo lengo lake lilikuwa kumpa mtaji wa kugombea ubunge na baada ya hapo unaibu uwaziri, uwaziri na uwaziri Mkuu. Alipokuwa anashukuru uwaziri Mkuu alikiri ya kuwa hajawahi kuzifanya kazi za uwakili au uhakimu au hata kuajiriwa kama mwanasheria katika maisha yake. Ya JK - haya yanahitaji kuchambuliwa kiundani zaidi kwani yumo kwenye kinyang’anyiro cha uraisi….

HISTORIA YA JK KITIJA HAITII MATUMAINI HATA KIDOGO.

Mara baada ya kumaliza Chuo Kikuu cha Dar-Es-Salaam JK alitua chamani ambako alivikwaa vyeo vya ukatibu wa wilaya na mkoa kwa msaada wa Bw. Kawawa (sasa hayati) ambaye alipokuwa ni katibu mkuu wa CCM. Kwenye uthibitisho wa mbeleko za Kawawa, JK alipokuwa anashukuru Mkutano Mkuu wa CCM mwaka 2005 kwa kuteuliwa kugombea uraisi alikiri ya kuwa bila ya kubebwa na mbeleko za Bw. Kawawa asingeliweza kufika hapo na alizitaja kwa uwazi kabisa mbeleko za Raisi Mstaafu Mwinyi ya kuwa zilichangia katika kumjenga kisiasa ingawaje JK alijisifia ya kuwa vipaji vyake va kisiasa ndivyo vimemfikisha hapo alipo!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!!
Kawawa kwa kuutumia wadhifa wake tajwa alimsukuma JK visiwani kama Katibu wa chama wa Mkoa ili kumfanya afahamike zaidi. Hili halikuwa dogo kwani baadaye kwenye vikao vya chama ambavyo huchagua viongozi wa kitaifa lilimsaidia JK kupata kuungwa na wanavisiwani na kuwabwaga wapinzani wake wa bara. Karata hii murua ya Mzee Kawawa ilikuwa ni lulu kwa JK. Katika vikao vya uteuzi wa wajumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM bara zile nafasi ishirini JK amekuwa akikamata nafasi tatu za juu kuanzia mwaka 1997 kutokana na mapungufu ya kimfumo tu ndani ya chama cha mapinduzi. Katika hali ya kawaida usingeliwategemea wanavisiwani kupiga kura kwenye teuzi za bara au wanabara kupiga kura kwenye teuzi za visiwani lakini ndani ya CCM hakuna kiongozi jasiri wa kutindua mfumo huu ambao umewapa nguvu bara kuwachagulia viongozi wanachama wa visiwani na kinyume chake.

Hizi ni mbeleko nyinginezo za kimfumo ambazo JK zilimpeperusha na kuonekana ni kiongozi anayekubalika ndani na nje ya bara hivyo afaa kufikiriwa kuwa Raisi wa Jamhuri wa Muungano wa Tanzania. Zaidi ya tathmini hii hakuna kiongozi yoyote yule zaidi ya Mzee Rukhsa ambapo alipokuwa anamnadi JK mwaka 2005 kule Tabora alidai bila ushahidi wowote kuwa katika uongozi wake JK ndiye aliyeanzisha taasisi ya kodi ya TRA wakati ukweli ni kuwa hayo yalikuwa mawazo ya Benki kuu ya Dunia. Mzee Rukhsa hakutaka kuzungumzia ya kuwa wakati wa JK misamaha ya kodi ilishamiri na hivyo kumfanya aliyemtangulia Bw. Kigoma Malima aonekane ni malaika. Mzee Rukhsa , vilevile, hakutaka wapiga kura wa Tabora waelewe ya kuwa JK alipokuwa waziri wa Nishati na madini, Tanesco ndiyo iliingia mikataba ya kitapeli ya IPTL na manunuzi yaliyokuja kufilisi Tanesco kwenye upatikanaji na uendeshaji wa mitambo ya uzalishaji wa umeme hapo Ubungo. Sababu za Mzee Rukhsa kuwadhulumu wapiga kura wa Tabora zipo dhahiri ya kuwa ni kuwaghilibu ili wasifanye maamuzi kulingana na utashi na mchango wa wagombea Uraisi waliokuwepo mbele ya macho yao mwaka huo wa 2005.
Utawala wa Mwinyi ambao mara nyingi ulikuwa unashutumiwa kwa udini wa kati ya mwaka 1995 hadi 2005 ndiyo haswa ulimteua JK kwenye nyadhifa za ubunge wa kuteuliwa na unaibu uwaziri na baadaye uwaziri. Hakuna tija yeyote ile iliyomwongoza Mwinyi katika uteuzi wa JK katika Wizara za fedha au Nishati na madini. Kutozingatia sifa katika teuzi za majukumu serikalini vilevile ni tatizo la kimfumo tu. Teuzi tajwa huwa hazichekechwi na Bunge huku Idara ya usalama hivi sasa hutumiwa kubariki teuzi tajwa kwa sababu hata walioko huko hawakuteuliwa kwa vigezo vinavyoheshimu tija. Jitihada hata za kuwashirikisha wananchi kupitia Bunge katika teuzi tajwa ni “njozi za alinacha” kwa sababu ambazo nitazifanunua hapo mbeleni. Kumbuka ya kuwa moja ya sababu za Dr. Slaa kugombea uraisi ni kupata ridhaa ya wananchi ya kurekebisha matatizo ya kimfumo ili kuongeza uwajibikaji wa dola kwa raia kupitia Bunge ambalo “utukufu” wake ghaghari utakoma tu kama tutamchagua Mheshimiwa Dr. Slaa hapo tarehe 31st October 2010 na wala siyo vinginevyo.

MADHARA YA JK KUWA KIONGOZI WA KUBEBWA KWENYE MBELEKO.

Viongozi wote duniani ambao wamesaidia nchi zao kutatua matatizo mengi yaliyokuwa yanawakabili wanahistoria ya kuwa waathirika wa mfumo uliokuwepo na hivyo kuwa na sababu za kimsingi za kuurekebisha na mifano ni kama ifuatavyo:-
(i) Uchina - Kiongozi aliyeleta mabadiliko makubwa ya kiuchumi alikuwa ni Deng Xiaoping huyu alifungwa na kiongozi aliyemtangulia - Bw. Mao Tsetung - miaka takribani tisa kwa sababu za kutofautiana naye kisiasa. Alipopata madaraka baada ya kifo cha Mao-Tsetung, Deng alileta mabadiliko makubwa ya kiuchumi ya kijani na leo Uchina inaendelea kunufaika na mabadiliko hayo miaka mingi baada ya Deng kuiaga dunia.
(ii) Huko Afrika Kusini, Mandela kwa takribani miaka ishirini na saba alisweka jela na makaburu lakini alipotoka na kupata nafasi ya kuiongoza nchi yake alijenga misingi ya utawala bora kwa kuandika katiba mpya yenye kuheshimu utu wa mtu ambao yeye aliukosa katika sehemu kubwa ya maisha yake.
JK hana historia ya mapambano au kuathirika na mfumo uliopo na ndio maana katika dhima zake hakuna mahali hata amethubutu kukemea tu matatizo ya kiuchumi yanatokana na mapungufu ya kimfumo hivyo kuwa na msukumo wa kuja na ajenda ya wazi ya kuurekebisha siyo tu kwa manufaa ya mwanawe Ridhiwani ila kwa manufaa ya vizazi vijavyo. Hili kwa JK halipo zaidi ya kutuahidi “tusahahu yaliyopita na tugange yajayo” kupitia kauli mbiu yake ya ARI ZAIDI, NGUVU ZAIDI NA KAZI ZAIDI YA UJENZI WA MIUNDO MBINU KWA UFADHILI WA MAREKANI!!!!!!!!
Kutokana na kuelewa hitilafu za kimfumo na changamoto zilizoletwa na utandawazi. Bw. Mkapa alipendekeza kwenye vikao vya juu vya CCM mrithi wake awe ni mtu anayefahamu athari za utandawazi lakini JK na wapambe wake wakielewa ya kuwa hatakuwa na ubavu wa kupambana na akina Dr. Abdallah Kigoda au Prof. Mark Mwandosya walipinga na kutishia kuwa wanaweza kujitoa CCM kuhitimisha yale yaliyotokea kwa KANU mwaka 2002!!!!!!! Kwa JK sifa za mrithi wa Mkapa zilikuwa ni aliyepata malezi bora ndani ya chama ili akifufue kiwe kama enzi za Nyerere kazi ambayo ndani ya CCM wenyewe wanakiri imemshinda kulikoni!!!!!!! Mkapa kwa kuogopa kuachiwa chama hewa kama Bw. Arap Moi kule Kenya alisalimu amri kwa kundi la wanamtandao ambalo JK ndiyo kinara wao…na mengineyo yaliyofuata sasa yanaunda historia yenye utata mwingi ya taifa hili.Kutokana na JK kukosa malezi ya changamoto za utandawazi na badala yake kuwa mtaalamu wa kichama zaidi, kitaifa tumekumbana na kero zifuatazo ambazo kamwe hata tukimpatia JK miaka mia moja ijayo hataweza kuzitatua :-
a)Matatizo ya kimfumo yanayosababisha tuongozwe na viongozi wabovu JK hakuyashughulikia katika kipindi chake cha kwanza, hayamo kwenye Ilani ya uchaguzi ya chama chake (2010-2015) wala hayamo kwenye ahadi lukuki kwenye mikutano yake ya kampeni. Tatizo kubwa kuliko lote la JK ni la kiupeo zaidi ya mengineyo. Kutokana na upeo wake kuwa ni finyu basi pamoja na kuwa madarakani kwa miaka mitano bado haoni ya kuwa kwa kuelekeza nguvu zake kwenye ujenzi wa miundo mbinu anatanguliza mkokoteni kabla ya farasi na safari hiyo ni sawa sawa kabisa na kutwanga maji kwenye kinu. JK alipokuwa kwenye kadamnasi ya kampeni zake kule Kondoa alikiri ya kuwa serikalini kuna “mchwa” ambao wanakula fedha za umma akadai atawashughulikia lakini hakuelezea kwa namna ipi na lipi atalifanya ambalo miaka mitano iliyopita alishindwa kulifanya………….

b)Kuubeba mfumo uliopita ndiyo ajenda kubwa ya JK ya kuendelea na Uraisi kwa msimu mwingine. Hili linajionyesha pale ambapo anawakumbatia akina Lowassa, Mramba, Bw. Vijisenti na wengineo wengine. Kwa Lowassa, JK alidai hajaona kiongozi mahiri kuliko huyo pengine akimaanisha “RICHMOND” ni hoyeee au hata Nyerere kiuongozi hafui dafu kwa Lowassa!!!!!!!! Miaka mitano ijayo ya JK kama akifanikiwa kuchakachua kura basi ataendeleza yaleyale aliyorithi kwa viongozi waliomtangulia. JK ni kweli amebadilisha mfumo wa kupata viongozi wa katikati ndani ya CCM baada ya kuona wamarekani jinsi walivyoweza kumchagua OBAMA kutokana na mfumo wao lakini hakuwa na ujasiri wa kuutumia mfumo huohuo shirikishi kwenye nafasi yake ya kinyang’anyiro cha URAISI. Hili linatufunza ya kuwa JK anapoona masilahi yake yapo hatarini yupo tayari kupindisha demokrasia ili mradi tu afanikishe minajili yake ya muda mfupi.

c)JK pamoja ni msomi wa uchumi lakini kutokana na kutozifanya kazi za taaluma hiyo ujuzi wake ni wa makabrasha tu na wa kusikiliza ushauri feki na kuufanyia kazi lakini nchi haiwezi kumtegema kuwa mbunifu hata kidogo. Katika kipindi cha miaka mitano, tumetumbukia kwenye lindi kubwa la umasikini kama usahidi wa shilingi yetu ilivyoporomoka kwa zaidi ya asilimia mia moja tangu Mheshimiwa huyu akamate usukani. Uraro wa mapato vilevile ni pasua kichwa. Matumizi yetu ya bidhaa za nje umekuwa marudufu bila kurandana hata kidogo na uzalishaji na uuzaji wa bidhaa zetu kwenye soko la nje. Mbali ya athari za kimfumuko wa bei na kudorora kwa kipato la taifa letu aidha kinyume na mahitaji ya kikatiba tumetumbukia katika kuishi kwa mikopo na misaada kutoka nje badala ya kujitegemea chini ya utawala wa JK. Hivi sasa JK haoni aibu kujivunia kuwa anaongoza taifa la ombaomba wakati nchi hii Mwenyezi Mungu ameipendelea sana kwa mali ghafi na watu wenye utashi mkubwa wa kisiasa.
d)JK, katika miaka mitano ya utawala wake taifa amelitumbukiza katika madeni makubwa. Mkapa alimwachia deni la karibu takribani Tshs trilioni 7 lakini yeye amekwisha kukopa zaidi ya TSHS Trilioni nane na ushee kidogo na kutusogeza kwenye deni la TSHS trilioni kumi na sita. Hoja zote za ahadi za JK kwenye eneo la miundo mbinu zitategemea huruma za wahisani ambao nao hivi sasa wamekamatwa pabaya na kamwe hawatakuwa na ubavu wa kushughulika na matatizo yetu huku wakijua ya kuwa uwezo wa kujitegema tunao ila ni wazembe wa kuchagua viongozi bora au kurekebisha mfumo wetu ili kupata viongozi bora ambao wanaroho ya kuthubutu na kujaribu mbinu nyingine za kuboresha tija.
KWA YEYEYOTE ATAKAYEMCHAGUA JK UKIIONDOA FAMILIA YAKE HAONI HIZI KASORO TAJWA HAZINA BUGHUDHA BASI BAADA YA KUMSIMIKA TENA JK HAPO IKULU ASILALAME NA UMASIKINI ………